Saturday, October 22, 2011

Kongamano la kijimbo Arusha mwaka 2012 SIKU 5


Leo 22/10/2011 kulikuwa na kikao cha Viongozi wa Viwawa Parokiani St.theresia Wajumbe walipendekeza siku ya kongamano la kijimbo na kufikia maamuzi kuwa kifanyike mwezi wa sita mwakani na kila mshiriki kuchangia kiasi cha sh 35,000 Tsh na kongamano litakuwepo mwezi wa sita kati 15.06.2012 up 24.06.2012 mwaka kesho,Na slogani ya kongamano kutoka katika muhubiri 12;1 au zaburi 199:9 Katika pesa hiyo ya 35,000 kila mshiliki hatapatiwa TISHETI YA KONGAMANO,Kongamano litakuwa la siku TANO kuanzia jumatano,LITAKUWA KONGAMANO Bora sana.

Thursday, October 20, 2011

Vijana jitaabisheni kuzifahamu Sakramenti za Kanisa: mwanzo, uponyaji, ushirika na huduma!

Mpendwa kijana, uchambuzi wetu wa Katekismu ya Vijana, YOUCAT, unatuingiza katika kuzichanganua Sakramenti Saba za Kanisa.
Kwa ujumla Sakramenti za Kanisa zinaweza kupangwa katika makundi makuu matatu. Kundi la kwanza ni la Sakramenti za Mwanzo, ambazo zinamwingiza mtu katika kupokea imani. Sakramenti za kundi hili ni tatu: Ubatizo, Kipaimara na Ekaristi Takatifu. Kundi la pili lina Sakramenti za Uponyaji: yaani Kitubio na Mpako wa Wagonjwa. Na kundi la tatu ni la Sakramenti za Ushirika na Huduma: hizi ni sakramenti ya Ndoa na Madaraja Matakatifu.
SAKRAMENTI YA UBATIZO ni sakramenti ya msingi na ufunguo wa sakramenti zote, ni agano ambalo mtu hanabudi kulikubali; ni njia ya kutoka katika ufamle wa mauti kuingia uzimani; na ni mwanzo wa muungano dumifu na Mungu. Ubatizo unaweza kufanyika kwa kumzamisha mtu mara tatu ndani ya maji au kwa kummwagiliwa maji kichwani mara tatu huku kukitamkwa “F… nakubatiza kwa jina la Baba, na la Mwana, na la Roho Mtakatifu.” Maji ya Ubatizo yanawakilisha maisha mapya na kutakatifuzwa katika Kristo. Ibada ya ubatizo hufungwa kwa kupakwa mafuta matakatifu, vazi jeupe na mshumaa wa ubatizo. Ubatizo unatolewa kwa mtu yeyote ambaye hajabatizwa.
Hitaji la lazima ili kubatizwa ni imani ambayo mtu anaiungama hadharani wakati wa ubatizo. Ubatizo hutolewa pia kwa watoto wachanga ambapo ungamo la imani hufanywa na wazazi kwa niaba ya watoto hao. Ukweli ni kwamba kabla mtu hajaitikiwa wito wa kubatizwa Mungu tayari amekwisha mkubali kuwa miongoni mwa watoto wake.
Na hivyo ubatizo ni neema, ni zawadi tusiyoistahili toka kwa Mungu. Kukubali Ubatizo wa mtoto mchanga kwa wazazi waamini ni tendo la upendo na matashi mema ya kumnasua toka dhambi ya asili na nguvu ya mauti. Mtu yeyote anapobatizwa anakuwa mshirika wa Mwili wa Kristo, kaka na dada wa Mwokozi, na mwana wa Mungu.
Kwa mtu yeyote aliyepokea Injili na kufahamu kuwa Kristo ni “njia, na kweli na uzima” (Yoh 14:6), Ubatizo ni njia pekee ya kwenda kwa Mungu na ya wokovu. Hata hivyo, kwa vile Kristo alikufa kwa ajili ya watu wote, wale wote ambao hawajapata nafasi ya kujifunza kumhusu Kristo na imani lakini wanamtafuta Mungu kwa dhamiri zao wanapata wokovu kwa ubatizo wa tamaa.
Kwa kawaida, Sakramenti ya Ubatizo huadhimishwa na Askofu, Padre au Shemesi. Lakini katika hatari ya kifo kila mkristo au mtu yeyote (hata asiye mkristo) naweza kubatiza kwa kutumia maji na kutamka maneno ya ubatizo: “F. Nakubatiza kwa Jina la Baba, na la Mwana, na la Roho Mtakatifu”. Anayebatiza hana budi kuwa na nia ya kutenda kile kinachofanywa na Kanisa linapobatiza.
Katika Ubatizo mtu hupokea jina jipya ikionesha kwamba Mungu mwenyewe amemuita kwa jina, anamfahamu, na hivyo ni wake. (Is 43:1). Mkristo huchagua jina la watakatifu ili kijipatia mfano wa kuigwa na kupata msaidizi, rafiki aliye kwa Mungu.
SAKRAMENTI YA KIPAIMARA inakamilisha ubatizo kwa kumpatia mwimarishwa zawadi ya Roho Mtakatifu kwa kuwekewa mikono; na kwa kupakwa mafuta matakatifu ya Krisma anapata nguvu ya kutoa ushuhuda wa upendo na uwezo wa Mungu kwa maneno na matendo. Mwimarishwa anakuwa mshirika kamili na mwajibikaji wa Kanisa Katoliki.
Katika Agano la Kale, watu walisubiri ujio wa Roho Mtakatifu juu ya Masiha. Na katika maisha yake, Kristo ameonesha kuwa na Roho wa upendo na muungano kamilifu na Baba. Huyu ndiye Roho aliyesubiriwa katika Agano la Kale, na ambaye Kristo aliwaahidia wafuasi wake; ndiye aliyewashukia wafuasi wake siku ya Pentekoste, na anayemshukia kila mmoja apateye Kipaimara.
Kinachofanyika wakati wa Kipaimara ni kwamba roho ya mkristo mbatizwa inapata muhuri usiofutika na unaomtambulisha mtu kuwa mkristo daima. Paji la Roho Mtakatifu linamwimarisha mtu kuwa shuhuda wa Kristo kwa maneno na matendo kupitia neema ya ubatizo.
Kipaimara kinaweza tu kutolewa kwa Mkristo Mkatoliki aliyebatizwa na aliye katika hali ya neema, yaani asiwe katika dhambi ya mauti. Kama mtu ametengana na Mungu kwa dhambi kubwa anapaswa kujipatanisha naye kwa kupokea Sakramenti ya kitubio. Sakramenti ya Kitubio inahitajika pia katika mazingira yote ambapo mtu anahitaji kujipatanisha na nafsi yake, na watu wengine, na Mungu, na kumkaribia Mungu hata kama hajatenda dhambi ya mauti.
Mwadhimishaji wa kawaida wa Sakramenti ya Kipaimara ni ASKOFU. Hata hivyo kama kuna sababu nzito na za lazima, Askofu anaweza kumruhusu padre atoe Kipaimara. Kunapokuwa na hatari ya kifo, padre yeyote anaweza kutoa kipaimara.
Kwa leo mpendwa kijana, naomba tukunje jamvi letu ili tuweze kujipatia muda wa kucheua haya tuliyopokea. Uchambuzi wetu wa Sakramenti saba za kanisa utaendelea wiki ijayo, siku na wakati kama huu. Nikikutakia kila jema, kutoka hapa Vatican, ni mtumishi wako, Padre Flavian Kassala.SOURCE kutokahttp://www.radiovaticana.org/EN3/articolo.asp?c=504225

Nyaraka za siri toka Vatican kuoneshwa hadharani, Februari, 2012 mjini Roma

 chanzo cha HABARI>>>www.radiovaticana.org
Kardinali Tarcisio Bertone, Katibu mkuu wa Vatican, Jumanne, tarehe 5 Julai, 2011 ameongoza jopo la viongozi waandamizi kutoka Vatican wakati wa kuwasilisha mkakati wa Vatican kushiriki katika onesho la Kumbu kumbu za Nyaraka za Siri za Vatican, litakalofanyika kwenye Jumba la Makumbusho la Jiji la Roma, hapo mwezi Februari, 2012.

Hii itakuwa ni mara ya kwanza kwa nyaraka za siri kutoka nje ya Vatican kwa ajili ya onesha la hadhara. Mkutano na waandishi wa Habari umehudhuriwa pia na Mstahiki Meya wa Jiji la Roma, Giovanni Alemanno na ujumbe wake.

Akizungumza na waandishi wa Habari, Kardinali Bertone anasema kwamba, tukio hili si la kawaida kwani linafanyika nje ya kuta za Vatican na litafanyika kwenye Jumba la Makumbusho la Roma, kitovu cha Jiji la Roma na utajiri wake unaofumbata uhusiano wa pekee na Vatican miaka nenda miaka rudi. Changamoto iliyokuwa mbele yao ni ile ya kuhakikisha kwamba, utajiri mkubwa, uzoefu na mang'amuzi yaliyoko kwenye nyaraka za siri za Vatican yanakwenda sanjari na matarajio ya Jiji la Roma.

Kwa upande wake, Kardinali Raffaele Farina, Mkutubi mkuu wa Vatican, alifafanua kwamba, nyaraka za kipapa zinazohifadhiwa kwenye Jumba la Kumbu kumbu za Nyaraka za Siri za Vatican ni muhimu sana katika maisha na utume wa Kanisa zima. Kwa mara ya kwanza, watu mbali mbali wanaweza kuzisoma nyaraka hizi ili kujichotea utajiri uliomo.

Askofu Sergio Pagano, Katibu mkuu wa Nyaraka za Siri za Vatican anasema, onesho hili linapania kutoa mwanga na uelewa mpana zaidi kuhusu asili na yaliyomo kwenye nyaraka hizi za siri zinazohifadhiwa katika Kumbu kumbu za Siri za Vatican, ndiyo maana onesho hili limepewa jina katika lugha ya Kilatini "Lux in Arcana" "Mwanga katika bahari". Kuna mammilioni ya nyaraka mbali mbali za Kanisa kutoka Vatican, kati ya hizo zote, Maktaba ya Vatican imeamua kuonesha nyaraka mia moja kwa wakati huu. Hali hii inaonesha kazi kubwa inayopaswa kufanywa ili kuwezesha umati mkubwa kushuhudia na kujisomea nyaraka hizi za Siri kutoka Vatican.

Kati ya nyaraka zitakazooneshwa ni ile ya Baba Mtakatifu Gregory wa Saba aliyeishi kunako mwaka 1073 hadi 1085; Barua ya Baba Mtakatifu Clementi wa Saba kwa Mfalme Henri wa nane kuhusu mgogoro wa ndoa, iliyoandikwa kunako mwaka 1530. Bila shaka wengi wangependa kufahamu kilichoandikwa na Kanisa wakati wa mashitaka ya Galileo Galilei kunako mwaka 1616 hadi mwaka 1633.

Askofu Pagano anasema, kwa mara ya kwanza, umma utapata fursa ya kujionea, kujisomea na kujichotea utajiri mkubwa unaofumbatwa katika Nyaraka za Siri za Vatican. Maendeleo ya teknolojia ya habari yatawawezesha watazamaji kuingia katika undani wa nyaraka hizi za kipapa na kufanya tathmini ya kina kuhusu mchango wake kwa maisha na utume wa Kanisa; katika masuala ya maisha, tamaduni, ujuzi na maarifa.

Mstahiki Meya wa Jiji la Roma Giovanni Alemanno anasema, Jiji la Roma linaona fahari kubwa kuweza kuwa ni mwenyeji wa onesho hili la pekee, hali inayoonesha uhusiano wa karibu kati ya Vatican na Jiji la Roma katika maisha ya kiroho na kimwili. Tukio hili ni kielelezo cha ushupavu na uwazi wa Vatican kuweza kuonesha nyaraka za Siri, nje ya kuta za Vatican. "Lux Arcana" hapo Februari, 2012, itakuwa ni fursa nyingine kwa mahujaji kujionea utajiri uliomo kwenye Nyaraka za Siri za Vatican na hija ya maisha ya mwanadamu: kiroho na kimwili.